UPENDO WA MUNGU KWETU
Baba wa mbinguni anatupenda si kwa
sababu Kristo alikufa kwa ajili yetu; bali alimtoa mwana wake kufa kwa sababu
anatupenda. Kupitia kwa Kristo Mungu alimimina pendo lake lisilo kifani kwenye
ulimwengu uliojawa na dhambi. “yaani, Mungu
alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie
makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho” 2 Kor 5:19. Kupitia maumivu
ya Gethsemani na kifo cha msalaba, Mungu alilipa gharama ya ukombozi wetu.
Yesu alisema, “Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena”
Yohn 10:17. Hii ni kusema kwamba, “Baba yangu aliwapenda mno kiasi cha
kunipenda mimi zaidi pale nilipoutoa uhai wangu kuwakomboa. Nalikufa badala
yenu, nilichukua dhabi zenu. Kwa sababu hii, nimekuwa karibu zaidi na Baba
yangu kuliko awali, na hata sasa Mungu bado anaokoa wenye dhambi wote
waniaminio.”
Kwa kumtoa mwanawe kufa kwa ajili
yetu, Baba yetu wa mbinguni alitoa kafara kuu na kulipa gharama ya wokovu wetu.
Gharama hii kubwa yapaswa kutusaidia kuelewa kile Mungu anachotegemea sisi kuwa
kupitia kwa Kristo.
Mtume Yohana aliona jinsi kimo, kina
na mapana ya upendo wa Mungu vilivyo. Alijaribu kuuzungumzia lakini hakuweza kuwa
na maneno sahihi ya kuuelezea, na hivyo akasema, “Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa
Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa
haukumtambua yeye.” 1 Yohn 3:1. Sisi ni wa thamani kiasi gani!
Kwa kufikiri juu ya upendo wa Mungu
tunanyenyekezwa. Wazo hili, kama lilivyooneshwa na kifo cha Yesu, linapaswa
kusogeza akili zetu karibu na Mungu. Kwa kadri tunavyojifunza tabia ya Mungu na
kudumu kuutazama msalaba, ndivyo tunavyozidi kuona rehema, upole na msamaha wa
Mungu. Ndivyo pia tunavyoona Mungu ni wa haki kiasi gani. Pia tunaona upendo
wake usio na mwisho na huruma yake inayozidi huruma ya mama kwa mtoto asiye
mtiifu.

No comments:
Post a Comment