Wednesday, October 11, 2017

JE UNAMJUA MUNGU?

JE UNAMJUA MUNGU?

“Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi;” Yohana 10:14
K


atika sura ya 3 ya kitabu cha 1 Samweli, tunapata habari za kuitwa kwa nabii Samweli tangu akiwa mtoto. Samweli alikuwa ni mtoto wa ahadi aliyetolewa wakfu kwa Mungu. Ijapokuwa alitolewa wakfu kwa Mungu na alikuwa akifanya kazi hekaluni, Samweli hakumjua BWANA, tena hakuitambua sauti ya BWANA.


“Basi Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake. Bwana akamwita Samweli mara ya tatu. Naye akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Ndipo Eli akatambua ya kuwa Bwana ndiye aliyemwita yule mtoto”. 1 Samweli 3: 7-8


Swali kwetu leo: Je, tunamjua Mungu? Je, tunamtambua? Tunasikiliza sauti gani katika maisha yetu? Mungu anapozungumza nasi Je, tunaitambua sauti yake?




Ni hatari sana kuwa kwa BWANA na wakati hatuijui sauti yake kwa maana ni rahisi kuifananisha na sauti nyingine. Samweli aliifananisha sauti ya BWANA na sauti ya kuhani Eli.


Kitu kizuri cha kutia moyo ni kwamba, ijapokuwa hakumtambua BWANA, Samweli alikuwa tayari kujifunza kuhusu Mungu.


“Bwana akaja, akasimama, akaita vile vile kama kwanza, Samweli! Samweli! Ndipo Samweli akasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia”. 1 Samweli 3:10




Swali kwetu leo: Je, ni mara ngapi tunatafuta kumjua BWANA kupitia neno lake?




Pasipo kusoma neno, kuna hatari ya kupoteza mwelekeo na hivyo kutomtambua BWANA.




Pia katika kitabu cha Matendo 9 kuna kisa cha Sauli aliyebadilika na kuwa Paulo. Sauli alijifuza elimu ya dini vizuri na kufikia kiwango cha mafarisayo. Watu walimwamini na kutegemea makuu toka kwake. Wengine walimtegemea kama kiongozi mkuu na mfundishaji mzuri wa elimu ya dini katika jamii ya wayahudi.


Kisha Sauli alipewa kazi ya kuwatafuta, kuwatesa na kuwaua watu wa Mungu walioonekana kuwa wazushi. Sauli alidhani kuwa anafanya kazi ya BWANA, kumbe alikuwa akimwudhi. Sauli hakutambua sauti ya BWANA. Ijapokuwa hakumtambua BWANA, alipoisikia sauti yake ikisema naye, alikubali na kuwa na utayari wa kumpendeza na kumtii.


Huenda kwetu mimi na wewe, isingetosha kwa kuisikia sauti tu, kuamini kwamba ni sauti ya Mungu.


Yohana 10:14 inasema “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi.”


Swali kwetu leo: Je, Mungu anatujua kama tulio wa kwake? Je, Mungu anatujua kama alivyomjua Ayubu, Daudi, Ibrahimu n.k.?


BWANA ameweka kila njia ya sisi kumfahamu Yeye. Tunao uchaguzi, BWANA halazimishi tumfahamu ila anataka tumfahamu. Ametupatia neno, alilipa deni kwa ajili yetu, ametupa Roho wake kutusaidia na anaendelea kutuombea.


Ikiwa tutatumia muda mwingi kutazama, kusikia na kusimulia kwa uzuri habari za dunia kuliko kutafuta habari za Yesu, macho yetu ya kiroho yatafumbwa na kamwe hatutaweza kumtambua BWANA.


Mathayo 11:28-29 inasema “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu”


Tunaye mchungaji mwema Yesu Kristo anataka kutuongoza na kubadili maisha yetu. Yesu anatuita sote kujisalimisha kwake. Kwake tutajifunza na kupata raha nafsini mwetu.





Sunday, September 10, 2017

FADHILI ZA BWANA



Kama tutasikiliza tu, basi, viumbe vilivyoumbwa na Mungu vitatufundisha mafundisho ya thamani juu ya utii na kumtegemea yeye. Kuanzia na nyota ambazo zinafuata njia zao zisizo na alama katika anga za juu na kizazi kwa kizazi zinafuata njia yao ziliyowekewa, mpaka chini kwenye atomu ndogo kabisa, viumbe vya asili huyatii mapenzi ya Muumbaji. Tena Mungu hukitunza na kukilisha kila kitu alichokiumba. Yule anayeyashikilia malimwengu yasiyohesabika katika eneo kubwa sana, wakati uo huo anajali mahitaji ya shomoro mdogo wa kikahawia aimbaye wimbo wake mdogo pasipo hofu.


Wanadamu wanapoondoka asubuhi kwenda kazini, na wakati waombapo; wakati wanapokwenda kulala usiku; na wakati wanapoamka asubuhi; tajiri anapofanya karamu katika jumba lake, au maskini anapowakusanya watoto wake kukizunguka chakula chao kidogo, kila mmoja huangaliwa kwa huruma na upendo na Baba yetu aliye mbinguni. Hakuna chozi limtokalo mtu ambalo Mungu halioni. Hakuna tabasamu yo yote asiyoiona.


Kama tungesadiki hivyo kabisa, mahangaiko yote yasiyofaa yangeondolewa mioyoni mwetu. Maisha yetu yasingejazwa na kukata tamaa mno kama yalivyo sasa; kwa sababu kila kitu, kiwe kikubwa au kidogo, kingeachwa mikononi mwake Mungu, ambaye hachanganyikiwi kuona ongezeko kubwa la masumbufu yetu, wala halemewi na mizigo yake. Hapo ndipo tungeweza kuifurahia amani mioyoni mwetu ambayo kwa wengi kwa muda mrefu imekuwa kitu kigeni.


Mungu husema nasi katika matendo yake na uongozi wake, tena katika mvuto wa Roho wake mioyoni mwetu. Katika mambo yanayotokea kwetu, na katika mazingira yetu, katika mabadiliko yanayotokea kila siku pande zote, twaweza kupata mafundisho ya thamani, kama mioyo yetu imekuwa wazi kuyatambua mafundisho hayo. Mtunga Zaburi, akifuatilia matendo na uongozi wa Mungu, asema hivi, “Nchi imejaa fadhili za Bwana.” “Aliye na hekima na ayaangalie hayo, na wazitafakari fadhili za Bwana.” Zaburi 33:5; 107:43.

_Njia Salama Sura ya 10.

Kama umebarikiwa na ujumbe huu na ungependa kujifunza zaidi, waweza kuweka comment hapo chini au kuwasiliana nasi kupitia ilalasda@gmail.com
 

Thursday, September 7, 2017

KIONGOZI SALAMA

KIONGOZI SALAMA

"Basi Yesu akawaambia tena akasema, Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa nuru ya uzima". Yohana 8:12.
 
Wote wanaosafiri katika njia ile iendayo mbinguni wanahitaji kuwa na kiongozi salama. Hatupaswi kwenda kwa kufuata hekima ya kibinadamu. Ni haki yetu kuisikiliza sauti yake Kristo ikisema nasi tunaposafiri katika safari ya maisha yetu, na maneno yake daima
ni maneno ya hekima....
Shetani anafanya kazi yake kwa juhudi kubwa sana ili kuzizingira na kuziangamiza roho za wanadamu. Ameshuka chini kwa nguvu nyingi, akijua kwamba anao wakati mchache tu wa kufanya kazi yake. Usalama wetu pekee ni kumfuata Kristo kwa karibu sana,
kutembea katika hekima yake, na kuitenda kweli yake. Hatuwezi kuutambua siku zote kwa upesi utendaji wake Shetani; hatujui ni wapi anapotega mitego yake. Lakini Yesu anazifahamu hila za chini chini za adui huyo, naye anaweza kuilinda miguu yetu ipate
kubaki katika njia zile zilizo salama.... "Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima" (Yohana 14:6) Yesu asema. ----- Letter 204, 1907.
Ingekuwa na faida gani njia ile ya moja kwa moja na ya hakika iendayo kule kwenye utukufu, kama pasingekuwako na nuru yo yote ya ile kweli ambayo ingeiangazia njie ile, ili wasafiri wapate kuitamani? Nuru inayoiangazia njia ile ingekuwa na faida gani kama uzima usingekuwamo ndani ya watu wale wanaosafiri katika njia ile, yaani, katika safari ile ya wasafiri kutoka duniani kwenda mbinguni? Wakiwa na usemi ule wa Kristo,usemao, "Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima," wale wote wanaomwamini Yesu, kiongozi wao, wanaweza kutembea kwa imani kwenda mbinguni, wakiwa na hakikakwamba wamo katika njia ile iliyoelezwa katika neno lake kuwa ndiyo njia. ----- Letter
63, 1893.
Wale waendao kwa utii wataijua kweli ilivyo.... Ili kuijua kweli, yatupasa kuwa tayari kutii. Wale ambao mapenzi yao yako katika mambo ya dunia hii hawako tayari kuiacha mipango yao kwa ajili ya mipango ya Kristo. Wanakwenda gizani, wasijue waendako.
Nuru ya thamani ya ile kweli huangaza ghafula juu ya njia ya kila mmoja anayeitafuta. --
--- MS 31, 1886.

Wednesday, September 6, 2017

MAOMBI



 

MAOMBI

MUNGU huzungumza nasi kupitia katika viumbe vyake vya asili na mafunuo
yake, kupitia katika maongozi yake, na kwa njia ya Roho wake. Lakini njia hizo
hazitoshi; sisi pia tunahitaji kumfungulia mioyo yetu. Ili tupate uzima wa kiroho na
nguvu yake, hatuna budi kuongea na Baba yetu aliye mbinguni. Mawazo yetu yanaweza
kuvutwa kwake; tunaweza kuzitafakari kazi zake, rehema zake, baraka zake; lakini
hayo, kwa maana yake kamili, si kuongea naye. Ili tuweze kuongea na Mungu, ni sharti
tuwe na mambo fulani ya kumwambia hasa kuhusu maisha yetu tunayoishi.

Katika kuomba tunamfunulia Mungu mioyo yetu na kuongea naye kama
tunavyoongea na rafiki wa kweli. Si lazima kufanya hivyo ili kumjulisha Mungu hali
yetu ilivyo, bali kuongea naye kunatuwezesha kumpokea mioyoni mwetu. Maombi
hayamlazimishi Mungu kushuka kwetu, bali ni sisi ambao tunainuliwa mpaka kufika
kwake.

Yesu alipokuwapo hapa duniani, aliwafundisha wanafunzi wake kusali.
Aliwaagiza waweke mahitaji yao ya kila siku mbele za Mungu, na kumtwika mizigo yao
yote. Na ahadi ile aliyowapa kwamba dua zao zingesikilizwa ni ahadi iliyotolewa kwetu
pia.

Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa;
kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa (Mathayo 7:7,8).