Wednesday, October 11, 2017

JE UNAMJUA MUNGU?

JE UNAMJUA MUNGU?

“Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi;” Yohana 10:14
K


atika sura ya 3 ya kitabu cha 1 Samweli, tunapata habari za kuitwa kwa nabii Samweli tangu akiwa mtoto. Samweli alikuwa ni mtoto wa ahadi aliyetolewa wakfu kwa Mungu. Ijapokuwa alitolewa wakfu kwa Mungu na alikuwa akifanya kazi hekaluni, Samweli hakumjua BWANA, tena hakuitambua sauti ya BWANA.


“Basi Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake. Bwana akamwita Samweli mara ya tatu. Naye akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Ndipo Eli akatambua ya kuwa Bwana ndiye aliyemwita yule mtoto”. 1 Samweli 3: 7-8


Swali kwetu leo: Je, tunamjua Mungu? Je, tunamtambua? Tunasikiliza sauti gani katika maisha yetu? Mungu anapozungumza nasi Je, tunaitambua sauti yake?




Ni hatari sana kuwa kwa BWANA na wakati hatuijui sauti yake kwa maana ni rahisi kuifananisha na sauti nyingine. Samweli aliifananisha sauti ya BWANA na sauti ya kuhani Eli.


Kitu kizuri cha kutia moyo ni kwamba, ijapokuwa hakumtambua BWANA, Samweli alikuwa tayari kujifunza kuhusu Mungu.


“Bwana akaja, akasimama, akaita vile vile kama kwanza, Samweli! Samweli! Ndipo Samweli akasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia”. 1 Samweli 3:10




Swali kwetu leo: Je, ni mara ngapi tunatafuta kumjua BWANA kupitia neno lake?




Pasipo kusoma neno, kuna hatari ya kupoteza mwelekeo na hivyo kutomtambua BWANA.




Pia katika kitabu cha Matendo 9 kuna kisa cha Sauli aliyebadilika na kuwa Paulo. Sauli alijifuza elimu ya dini vizuri na kufikia kiwango cha mafarisayo. Watu walimwamini na kutegemea makuu toka kwake. Wengine walimtegemea kama kiongozi mkuu na mfundishaji mzuri wa elimu ya dini katika jamii ya wayahudi.


Kisha Sauli alipewa kazi ya kuwatafuta, kuwatesa na kuwaua watu wa Mungu walioonekana kuwa wazushi. Sauli alidhani kuwa anafanya kazi ya BWANA, kumbe alikuwa akimwudhi. Sauli hakutambua sauti ya BWANA. Ijapokuwa hakumtambua BWANA, alipoisikia sauti yake ikisema naye, alikubali na kuwa na utayari wa kumpendeza na kumtii.


Huenda kwetu mimi na wewe, isingetosha kwa kuisikia sauti tu, kuamini kwamba ni sauti ya Mungu.


Yohana 10:14 inasema “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi.”


Swali kwetu leo: Je, Mungu anatujua kama tulio wa kwake? Je, Mungu anatujua kama alivyomjua Ayubu, Daudi, Ibrahimu n.k.?


BWANA ameweka kila njia ya sisi kumfahamu Yeye. Tunao uchaguzi, BWANA halazimishi tumfahamu ila anataka tumfahamu. Ametupatia neno, alilipa deni kwa ajili yetu, ametupa Roho wake kutusaidia na anaendelea kutuombea.


Ikiwa tutatumia muda mwingi kutazama, kusikia na kusimulia kwa uzuri habari za dunia kuliko kutafuta habari za Yesu, macho yetu ya kiroho yatafumbwa na kamwe hatutaweza kumtambua BWANA.


Mathayo 11:28-29 inasema “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu”


Tunaye mchungaji mwema Yesu Kristo anataka kutuongoza na kubadili maisha yetu. Yesu anatuita sote kujisalimisha kwake. Kwake tutajifunza na kupata raha nafsini mwetu.





No comments:

Post a Comment